CHANGAMOTO INAYO IKUMBA HIFADHI YA MLIMA KILIMANJARO

Picha ikionesha muonekano wa Mlima Kilimanjaro katika kituo cha Shira cave mita 3750 toka usawa wa bahari.

MOSHI.

IMEELEZWA kuwa mabadiliko ya tabia nchi yameathiri viumbe hai pamoja na uchumi wa Taifa huku wanyama pori wakiwa katika hatari ya kutoweka kutokana na uharibifu na shughuli za kibinadamu.


Hayo yamebainishwa na  Kaimu mkurugenzi Mkuu wa TANAPA Mtango Mtahiko wakati akifungua warsha ya siku tatu ya uhifadhi kwa waandishi wa habari mkoa Kilimanjaro iliyo fanyika Mjini Moshi.

Amesema kuwa  hifadhi 16 zilizopo chini ya TANAPA zina kabiliwa na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi kutokana na athari zinazo tokana na shughuli za kibinadamu ambazo siyo rafiki kwa mazingira kama vile uchomaji mkaa ndani ya hifadhi,kilimo ndani ya hifadhi,ufugaji ndani ya hifadhi  na uharibifu wa vyanzo vya maji ndani ya hifadhi licha ya TANAPA kufanya jitihada za kuondoa changamoto hizo kwa kutoa elimu kwa jamii zinazo zunguka maeneo ya hifadhi.

Mtahiko amesema kuwa Waandishi wa habari wanajukumu la kuhakikisha kuwa wananchi wanapata na kupokea habari muhimu za kutunza mazingira yanayo hifadhiwa ili kuweza kujenga kizazi kitakacho yachukulia mazingira kuwa ni muhimu kwao na kuachana na uharibifu wa mazingira yatakayo pelekea ukiwa kwa viumbe hai.

Ameongeza kuwa  hali ya Barafu katika kilele cha mlima  Kilimanjaro imezidi kupungua kutokana na changamoto alizozitaja hivyo kupelekea mabadiliko ya tabia nchi kwa kupokea mvua kidogo,joto na maeneo mengine kukosa mvua kabisa.

Naye Afisa uhusiano toka TANAPA Pascal Shelutete amebainisha kuwa hifadhi ya mlima Kilimanjaro na Hifadhi ya serengeti zimekuwa zikijiendesha zenyewe kwa kutoa gawio lake kwa serikali tofauti na hifadhi nyingine duniani zinazo tegemea kupata ruzuku toka serikalini,kutokana na usimamizi mzuri unao fanywa kuhakikisha kuwa sekta ya uhifadhi inafanya kazi kwa faida .

Akizungumzia kuhusu migogoro ya mipaka Shelutete amekiri kuwa kumekuwa na tatizo la migogoro ya mipaka katika baadhi ya hifadhi na wananchi wanao zunguka hifadhi,ambapo tatizo hilo linaweza kuvunja uhusiano mzuri uliopo kati ya shirika na wananchi,licha ya jitihada mbalimbali kuchukuliwa na TANAPA kuondoa tatizo hilo.

Katika hatua hiyo Shelutete amewataka wanahabari kutumia kalamu zao vizuri katika kutoa elimu kwa wananchi,juu ya umuhimu wa kuhifadhi na kutembelea hifadhi za taifa kwaajili ya kujifunza na kufurahia urithi huo wa asili,ili kujenga kizazi kitakacho endeleza jitihada hizo za uhifadhi.

Warsha hiyo ya Uhifadhi  kwa waandishi wa habari ilifanyika kwa siku tatu mjini Moshi ikiwa ni sambamba na wanahabari hao kutembelea kambi ya Shira Cave kuona utalii wa uokoaji.